BIASHARA 10 ZA MTAJI MDOGO ZENYE FAIDA KUBWA
Tuangalie biashara 20 za mtaji mdogo usiozidi Tshs. 100,000 unazoweza kufanya na zenye faida kubwa. Mtaji mkubwa unaohitajika unapoanzisha biashara ni muda na wala sio pesa kama utakavyojifunza hapa.
Hakuna biashara ndogo, ila kuna biashara unazoweza kuanza na mtaji mdogo na zikakuletea faida kubwa. Hiyo ambayo inaitwa “biashara ndogo” ukiifanya kwa ubora wa hali ya juu na bidii ipo siku itakutoa.
Kabla hatujaenda kwenye hiyo orodha ya hizo biashara za mtaji mdogo, hebu tuweke sawa kauli ya “zenye faida kubwa”. Faida kubwa haimaanishi mamilioni ya fedha, bali ni kwamba faida utakayoipata kulingana na mtaji wako ni nzuri na usipokata tamaa itakufikisha mbali.
ZINGATIA:
Unapotaka kuanzisha biashara yoyote ile, ni vyema kufuatilia utaratibu na sheria za mahali ulipo. Tafadhali ilinde biashara yako kwa kufuata kanuni zote zilizowekwa na serikali ambazo unaweza kuzikamilisha bila usumbufu wowote na kwa gharama nafuu sana.
Baada ya kulisawazisha hilo, twende kwenye hiyo orodha ya biashara za mtaji mdogo kama zifuatazo;
1. KUPIKA KWA ODA
Kama wewe ni mpishi mzuri au una mtu anayejua kupika, basi jitangaze kama unapokea oda za mapishi fulani. Tuchukulie unaweza kupika makande au wali nyama vizuri.
Unachoweza kufanya ni kwenda maofisi ya karibu yako na kuwaambia kwamba wakutafute wanapohitaji hicho chakula wakati wa mchana na wewe utawaletea. Usisahau kuacha mawasiliano yako ili waweze kukutafuta. Wengi wao watapenda hiyo huduma kwasababu hawatohitaji kutoka tena kufata chakula.
2. UREMBO (MAKEUP, KUSUKA & KUCHA)
Urembo ni gharama. Wanadada wanataka kupendeza wanapokwenda safari zao kama ni kazini ama shughulini. Uzuri ni kwamba hii ni biashara ya kila siku unayoweza kufanya. Baada ya kufanya utafiti wangu, nimebaini kwamba kufanya makeup, kutengeneza kucha na ususi wa nywele zinalipa vizuri tu. Kuna watu wengi tu wanaendesha maisha yao kupitia biashara hizo. Kwanini wewe ushindwe? Na kama sio mtaalamu, hakuna tatizo. Chukua muda wako na kujifunza, ndani ya muda utaweza.
3. KUUZA JUISI NA ICECREAM
Kujifunza kutengeneza juisi au icecream haitakuchukuwa muda mrefu. Ili kufanikiwa katika biashara hii, cha muhimu ni kujitofautisha. Muhimu zaidi unapofanya biashara ya kutengeneza juisi au icecream, ni kuweka mazingira yako safi na salama kwa wateja wako. Uzuri wa biashara hii ni kuwa mtaji wake ni mdogo sana. Elfu kumi tu inatosha kuanzia na wapo waliofanya hivyo na wamekuza biashara zao kama vile Mak Juice au Zanana Juice Box.
4. KILIMO CHA MBOGAMBOGA
Kilimo ni sehemu kubwa ya maisha ya watanzania na wale wa nchi nyingi za Afrika. Kila siku zikienda, kilimo huzidi kuwa ni biashara ya matajiri kwasababu shamba lina gharama kubwa. Licha ya hivyo, bado kuna fursa ya kutengeneza kipato kupitia kilimo cha mbogamboga hata kama una mtaji mdogo. Anza na sehemu ndogo tu unayoweza kupata hata kama ni nyumbani.
5. UFUGAJI WA NDEGE (KUKU, BATA, N.K)
Hii ni biashara ambayo ina faida kubwa lakini pia ina changamoto zake kama vile kuku wako kufa. Vifo vya mifugo huwaumiza sana wafugaji na mara nyingi husababishwa na mifugo hiyo kula uchafu. Hivyo, unapoingia kwenye ufugaji jitahidi uwe na mazingira safi na salama kwa mifugo yako. Usafi wa mara kwa mara hasa hasa kwenye malisho yao utahitajika. Kwa vile mtaji ni mdogo, unaweza kuanza na kuku wa kienyeji, bata au hata njiwa. Japo kuwa wanachukuwa muda ila kuwa mvumilivu, faida utaiona.
6. KUTENGENEZA TOVUTI (WEBSITES)
Tuko katika ulimwengu wa habari na teknolojia, hivyo kampuni ama biashara ambayo hawako mtandaoni wanakosa wateja. Ichangamkie fursa hiyo kwa kujifunza kutengeneza websites kupitia YouTube. Kisha, tafuta biashara/ makampuni ambayo hawana tovuti na uwaelezee umuhimu wa kuwa na tovuti. Mwisho, waambie kuwa wewe unatoa huduma hiyo. Kwa kuanza, wateja wako wa mwanzo unaweza kuwafanyia kwa bei ya punguzo halafu mbeleni ukapandisha. Njia hii itakusaidia kupata mabalozi watakao kupatia wateja wengine.
7. KUPANGA SHEREHE/MATUKIO (EVENT PLANNING)
Kuanzia maharusi, kitchen party, send - off na sherehe nyenginezo nisizozifahamu. Zote hizi ni fursa ambapo unaenda kusaidia watu kuandaa sherehe zao mwanzo mpaka mwisho. Wewe ndio unaumiza kichwa kutafuta watu na huduma mbalimbali kama vile wapambaji, ma DJ, au kuwatafutia gari ya kukodi, kuwapikia chakula na megine mengi. Unachohitaji kuweza kufanya biashara hii ni uwe unawajua watu husika wanaotakiwa kwenye sherehe hizo. Mfano, ujue wapambaji wa ukumbi, wapishi wa maharusi, ma-DJ ili uweze kuwapa kazi hizo. Utalipwa kwa kufanya kazi hiyo.
8. USHONAJI NGUO
Kama wewe ni mpenzi wa mitindo, unaweza tengeneza kipato kizuri kwa kuwashonea watu nguo. Itakuchukuwa muda kujifunza kushona ila ni kazi moja nzuri. Unapata kuwa mbunifu katika kutengeneza mishono mbali mbali na mwisho wake kulipwa. Kama huna cherehani nyumbani, unaweza kwenda kukodi na kufanyia kazi zako hadi utakapo nunua yako.
9. KUFUNDISHA
Unaweza kufundisha chochote kila unachokijua ikiwa kuna watu wanataka kujifunza. Jitathmini kwa kujiuliza, je ni kitu gani nakijua ambacho watu wanataka kujifunza? Hiyo ni rasilimali tosha. Watafute hao watu na uwape huduma zako. Taaluma sio lazima iwe kufundisha hesabati na kemia tu, kama unajua kupika vizuri, kushona au chochote kile basi wafundishe watu.
10. KUNUNUA NA KUUZA BIDHAA
Sifa ya kubwa ya mjasiriamali ni kuona thamani ya vitu kabla wengine hawajaviona. Hivyo, tafuta bidhaa ambazo zinauzwa kwa bei ya chini, zinunue na utafute soko ambalo hizo bidhaa zinauzwa kwa bei ya juu uende ukaziuze huko. Mfano, unaweza kutoa bidhaa Dar es Salaam ukaenda kuuza Mwanza na kinyume chake pia inawezekana.
Kama nilivyotangulia hapo awali kwa kusema; “hakuna biashara ndogo”. Kinachofanya biashara ifanikiwe sio pesa, ni kujifunza, bidii, mbinu na kutokata tamaa katika safari yako hiyo. Jasho na muda ndio mtaji mkubwa na kila kizuri kina changamoto zake. Hivyo, changamoto zitakapokuja kuwa na ujasiri wa kutafuta suluhisho lake. Ukiweza kufanya hivyo utapiga hatua. Amua kwa Busara. Karibu kwenye page yetu tujifunze masuala anuwai kuhusu Mahusiano, Biashara na maisha kwa ujumla.
.png)
Comments
Post a Comment